Pambano

Error message

  • Deprecated function: unserialize(): Passing null to parameter #1 ($data) of type string is deprecated in css_injector_init() (line 53 of /home/krwester/gobibletranslations.org/sites/all/modules/css_injector/css_injector.module).
  • Deprecated function: unserialize(): Passing null to parameter #1 ($data) of type string is deprecated in css_injector_init() (line 53 of /home/krwester/gobibletranslations.org/sites/all/modules/css_injector/css_injector.module).
(Matendo 15)
Swahili
Year: 
2017
Quarter: 
4
Lesson Number: 
2

Somo hili limetafsiriwa kutoka katika Copr. 2011, Bruce N. Cameron, J.D. Marejeo yote ya maandiko yametoka kwenye tafsiri ya New International Version (NIV), copr. 1973, 1978, 1984 International Bible Society, isipokuwa kama itaelezwa vinginevyo. Nukuu kutoka kwenye tafsiri ya Biblia ya NIV inatumika kwa ruhusa ya Wachapishaji wa Biblia wa Zondervan. Majibu yaliyopendekezwa yanapatikana kwenye parandesi (kwenye mabano). Somo limekaa kimtazamo kwamba mwalimu anatumia ubao au sehemu nyingine yoyote ambayo inaweza kuonekana na wanafunzi. Kama huwa una kawaida ya kupokea somo hili kwa njia ya barua pepe na hukulipata kwa juma moja, unaweza kulipata kwa kubofya kwenye www.lesoni.blogspot.com kwa lugha ya Kiswahili na http://www.GoBible.org kwa lugha ya Kiingereza pamoja na lugha nyingine kama vile Kifaransa, Kijerumani. Omba kwa ajili ya uongozi wa Roho Mtakatifu unapojifunza.

 

Utangulizi: Hii itakuwa na mshtuko. Somo letu juma hili, somo letu la pili katika mfululizo wa masomo ya Warumi, halina vifungu kutoka katika kitabu cha Warumi! Hiki ndicho tunachokifanya, na nadhani utakubaliana kwamba hili ni wazo zuri: kutusaidia kuelewa vizuri zaidi barua ya Paulo kwa Warumi tunajifunza utangulizi wa barua ya Paulo. Somo letu kuu ni kumbukumbu (maandishi) iliyopo katika Matendo 15 juu ya pambano kubwa kabisa katika kanisa la mwanzo la Kikristo. Hebu tuzame kwenye somo letu ili tujifunze zaidi!

 

  1. Maonesho

 

    1. Soma Matendo 15:1. Haya ni mashtaka makubwa sana – wokovu unageukia kwenye suala la tohara! Msingi wa madai haya ni upi? (“Desturi iliyofundishwa na Musa.”)

 

      1. Je, utaitegemea “desturi” katika teolojia yako?

 

        1. Je, ni kweli kwamba walikuwa wanaitegemea “desturi” tu? (Sidhani! Soma Mwanzo 17:9-10 na Mwanzo 17:12-14. Sasa tunaweza kuelewa madai ambayo wanaounga mkono suala la tohara wanayatoa, ya mtu kutokuweza kuokolew Mwanzo 17:14 inasema kuwa ikiwa hujatahiriwa, hata kama wewe ni “mgeni” uliye sehemu ya nyumba unamoishi, umevunja agano lako na Mungu na “utatengwa” na watu wa Mungu.)

 

    1. Soma Matendo 15:2. Paulo ana mtazamo gani juu ya suala hili? (Hakubaliani kwa nguvu zote.)

 

      1. Wanashauri nini katika kutatua mabishano haya? (Kwa kuyapeleka kwa uongozi wa kanisa.)

 

      1. Mojawapo ya miongozo ya Urejeshaji wa Uprotestanti ni “ukuhani wa waumini wote.” (Angalia 1 Petro 2:9.) Kwa nini Paulo anakwenda kwa mitume na wazee kule Yerusalemu? Ninawafahamu watu wengi wanaobadili makanisa kisa tu hawakubaliani na sera ya kanisa. (Mambo mawili. Kwanza, sera ya sasa bado ilikuwa haijaamuliwa katika kanisa la awali la Kikristo. Pili, Paulo asingeenda kwa uongozi wa kanisa endapo alidhani kuwa msimamo wa kanisa haukuwa wa muhimu. Kwa sasa ninasoma kitabu kinachojenga hoja kuwa wazo la kwamba kila mtu anaweza kuwa “papa” wa namna yake ni tatizo la kiteolojia. Bado sijafika mbali sana katika usomaji wa kitabu hiki kiasi cha kutoa maoni yangu juu ya hoja hii.)

 

    1. Soma Matendo 15:4-9. Msingi wa hoja ya Petro ni upi? Anadai mamlaka gani? (Kwamba Roho Mtakatifu aliyafunua mapenzi ya Mungu katika suala hili.)

 

 

      1. Unadhani Petro anazungumzia tukio gani? (Pitia kwa haraka haraka Matendo 10 ili ujifunze zaidi maono ya Petro darini kuhusu wanyama wasio safi na safari yake kwenda kwa Kornelio akida wa Kirumi. Soma Matendo 10:44-47. Nadhani hii ndio rejea ya Petro.)

 

      1. Tunatakiwa kutafakari jambo hili. Mwanzo 17 iko wazi kabisa na ni sehemu ya kifungu cha Biblia. Tofauti na hili, Petro anayategemea maono yake na utendaji kazi wa Roho Mtakatifu miongoni mwa wanadamu. Ungetoa uamuzi gani endapo ungekuwa miongoni mwa viongozi wa Yerusalemu? (Kwa ujumla, jambo hili lingenitia wasiwasi/woga. Neno liko wazi, na Mungu anasema kuwa habadiliki. (Yakobo 1:17).)

 

    1. Soma Matendo 15:10-11. Petro anajenga hoja gani hapa? (Hoja ya vitendo: hakuna awezaye kuzishika sheria zote. Anajenga hoja kwamba haki kwa imani ni sahihi, kwa kuwa “nira” ya sheria ni jambo ambalo Wayahudi hawajaweza kuibeba.)

 

    1. Soma Matendo 15:12. Hoja iliyomaanishwa na Paulo na Barnaba ni ipi? (Roho Mtakatifu anaidhinisha kwenda kwa wanafunzi kwa sababu anatia nguvu “ishara na maajabu” miongoni mwao.)

 

      1. Soma Yohana 10:25-27. Yesu alitumia miujiza kuthibitisha kuwa alikuwa Mwana wa Mungu. Je, miujiza inapaswa kuwa hitimisho la uthibitisho? (Soma onyo la Yesu katika Mathayo 24:24-25. Paulo ananukuu miujiza kama uthibitisho kwamba Mungu aliidhinisha kazi miongoni mwa Mataifa.)

 

    1. Tunazo hoja tatu zilizoandikwa: utendaji (kazi ya) wa Roho Mtakatifu, masuala ya kivitendo na miujiza. Hivi vinapingana na mafundisho ya wazi ya Biblia. Utaamua vipi endapo ungekuwa unakabiliana na aina hizo za hoja zinazopingana leo?

 

  1. Uamuzi

 

    1. Soma Matendo 15:13-18. Yakobo anaongezea nini kwenye hoja ya Petro? (Anaongezea sehemu ambayo ninaichukulia kuwa ni jaribio kubwa sana la hoja ya kiteolojia. Ananukuu maneno ya Biblia (Amosi 9:11-12) kuonesha kwamba Mungu alikusudia injili iwaendee Mataifa.)

 

    1. Soma Matendo 15:19-21. Nani anayezungumza kwa niaba ya uongozi wa kanisa? (Yakobo. “Ni wajibu wangu.”)

 

      1. Yakobo anafanyaje maamuzi? (Anakubaliana na hoja ya kutotahiri.)

 

      1. Angalia kwa makini hitimisho la Yakobo. Je, anapigia kura uongozi wa Roho Mtakatifu katika kupingana na kifungu cha Biblia? (Hapana! Ananukuu Biblia na uongozi wa Roho Mtakatifu katika uamuzi wa kanisa. Hili, nadhani, ni jambo la muhimu sana. Kuanzisha fundisho linalotegemea kwa asilimia zote madai ya uongozi wa Roho Mtakatifu, wakati fundisho la Biblia linakinzana, ni kosa. Hata hivyo, ikiwa Biblia haina uhakika, na ina ukinzani wenye hoja, basi Roho Mtakatifu ndio kimbilio kwa ajili ya hitimisho sahihi.)

 

 

      1. Kutokana na eneo hili lenye mgogoro, je, Mwanzo 17 ina mtafaruku na unabii kwamba injili itakwenda kwa Mataifa? (Mahakimu wa Kimarekani wanapotafakari kujua endapo kuna mgogoro usiosuluhishika kati ya sheria mbili, wanaangalia kama sheria zote mbili zinaweza kutekelezwa. Hapa, zote mbili zinaweza kutekelezwa. Unaweza kuruhusu injili iende kwa Mataifa na unaweza kuwataka watahiriwe.)

 

        1. Sisemi kwamba Yakobo pamoja na kanisa la awali walifanya uamuzi mbay Lakini kama niko sahihi kwamba hakuna mgogoro usiosuluhishika, tunajifunza nini leo katika kutatua migogoro mikubwa kanisani?

 

    1. Soma tena Matendo 15:20-21. Je, hivyo ndivyo? Mimi ni mtu wa Mataifa. Je, kundi hili la sheria za ajabu ndilo linalopaswa kutumika kwangu?

 

      1. Tafakari Amri Kumi. Soma Kutoka 20:3-6 na ulinganishe na Matendo 15:20. Kati ya matakwa yote ya kumwabudu (kumsujudia) Mungu peke yake na kutoziabudu sanamu, je, Mataifa wanatakiwa kuacha kula nyama zinazotolewa kafara kwa sanamu pekee? Mwingiliano mwingine wote na miungu ni sawa? (Hitimisho hili ni la mzaha sana kuweza kulikubali. Unapoangalia orodha finyu anayoibainisha Yakobo, inaonekana kwamba anaelezea matumizi finyu ya sheria ya mapokeo iliyotolewa kupitia kwa Musa. Rejea mahsusi katika Matendo 15:21 kwa Musa kusomwa katika masinagogi inatilia mkazo wazo hilo.

 

    1. Soma Matendo 15:22-23. Hii inatuambia nini juu ya mamlaka ya hitimisho la Yakobo? (Huu ni uamuzi wa uongozi wa Kanisa la awali la Kikristo.)

 

    1. Hebu tusome barua rasmi katika Matendo 15:24-29. Hitimisho ni lipi kuhusu suala la tohara? (Kwa dhahiri, tohara haipo kwenye matakwa yaliyoorodheshwa.)

 

      1. Unadhani kwa nini tohara hata haikutajwa kwenye barua? Kwa nini suala mahsusi ambalo mjadala huu umelengwa halikutajwa? (Soma tena Matendo 15:5. Suala halisi halikuwa tohara pekee, bali pia kuishika “sheria ya Musa.” Hivyo, barua rasmi ya maoni ilijumuisha masuala yaliyokuwa yanajadiliwa.)

 

      1. Unadhani inamaanisha nini kusema “sheria ya Musa?” (Ukipitia kwa haraka haraka Kutoka 19 na 20 utaona kwamba Mungu alitamka (Kutoka 20:1) Amri Kumi mbele ya watu. Sidhani kama mwanafunzi yeyote makini wa Biblia anaamini kuwa Musa alitunga kanuni na taratibu zilizopo kwenye vitabu vya Kutoka na Mambo ya Walawi. Zote zilitoka kwa Mungu. Lakini, ukweli kwamba Amri Kumi pekee zilitamkwa na Mungu moja kwa moja kwa wanadamu inaweza kujenga msingi wa hoja kwamba amri hizo si sehemu ya “sheria ya Musa.”)

 

    1. Soma Wagalatia 2:11-13. Wale wasomaji ambao mara kwa mara wanafuatilia masomo ya GoBible.org wanafahamu kuwa tumemaliza tu kujifunza barua ya Paulo kwa Wagalatia. Kuna mtafaruku gani tunaouona kwenye Wagalatia? (Suala lile lile! Petro hata yuko kwenye upande wa mambo usio sahihi kwa muda (temporarily.) Kifungu kinasema kuwa watu wanaounga mkono tohara walitoka kwa “Yakobo.” Tunaweza kuona hili lilikuwa suala kubwa katika kanisa la awali, hata wakati mwingine wahusika wakuu kutokuwa na uhakika.)

 

 

    1. Rafiki, unayaingilia vipi mambo ambayo panakuwepo na kutokukubaliana kanisani? Ikiwa hukubaliani na uongozi wa kanisa, mfano wa Matendo 15 unakufundisha nini? Suluhu ya Matendo 15 inafundisha nini juu ya vyanzo vya mamlaka ya kutafuta suluhu?

 

  1. Juma lijalo: Hali ya Kibinadamu.