Mada Kuu Katika Petro wa 1 na 2

Error message

  • Deprecated function: unserialize(): Passing null to parameter #1 ($data) of type string is deprecated in css_injector_init() (line 53 of /home/krwester/gobibletranslations.org/sites/all/modules/css_injector/css_injector.module).
  • Deprecated function: unserialize(): Passing null to parameter #1 ($data) of type string is deprecated in css_injector_init() (line 53 of /home/krwester/gobibletranslations.org/sites/all/modules/css_injector/css_injector.module).
(1 na 2 Petro)
Swahili
Year: 
2017
Quarter: 
2
Lesson Number: 
13

Somo hili limetafsiriwa kutoka katika Copr. 2011, Bruce N. Cameron, J.D. Marejeo yote ya maandiko yametoka kwenye tafsiri ya New International Version (NIV), copr. 1973, 1978, 1984 International Bible Society, isipokuwa kama itaelezwa vinginevyo. Nukuu kutoka kwenye tafsiri ya Biblia ya NIV inatumika kwa ruhusa ya Wachapishaji wa Biblia wa Zondervan. Majibu yaliyopendekezwa yanapatikana kwenye parandesi (kwenye mabano). Somo limekaa kimtazamo kwamba mwalimu anatumia ubao au sehemu nyingine yoyote ambayo inaweza kuonekana na wanafunzi. Kama huwa una kawaida ya kupokea somo hili kwa njia ya barua pepe na hukulipata kwa juma moja, unaweza kulipata kwa kubofya kwenye www.lesoni.blogspot.com kwa lugha ya Kiswahili na http://www.GoBible.org kwa lugha ya Kiingereza pamoja na lugha nyingine kama vile Kifaransa, Kijerumani. Omba kwa ajili ya uongozi wa Roho Mtakatifu unapojifunza.

 

Utangulizi: Tunafikia mwisho wa somo letu la nyaraka mbili za Petro kwa Wakristo wa awali na kwetu. Tumejifunza nini katika mfululizo wa masomo haya? Mara zote wanafunzi wangu katika shule ya sheria huwa wanataka tupitie upya kile tulichojifunza, hivyo hebu tupitie baadhi ya mada zinazohusu ushauri wa Petro kwetu!

 

  1. Maisha Halisi

 

    1. Soma Kumbukumbu la Torati 28:1-6. Jambo gani linaahidiwa kutokana na utiifu “kamili?”

 

    1. Soma Kumbukumbu la Torati 28:15-20. Nini kimeahidiwa kwa wale wasiomtii Mungu na wale wanaomtelekeza (wanaomtupa)?

 

    1. Soma 1 Petro 1:6-7. Hii inaendanaje na ahadi zilizotolewa katika Kumbukumbu la Torati? (Petro anatuambia kuwa kuna vipimo vya imani yetu visivyofuata vipimo vya kawaida.)

 

    1. Utaona kwamba 1 Petro 1:6 inaanza kwa kusema “Mnafurahi sana wakati huo.” Kufurahi katika jambo gani? Hebu tuchunguze hilo kwa kusoma 1 Petro 1:3-5. Je, hii inaelezea hali yetu ya sasa? (Petro anasema kuwa tunaweza kupata mateso sasa hivi, lakini wakati huo huo Mungu anatukinga wakati tunapoutazamia uzima wa milele mbinguni.))

 

      1. Hebu subiri kidogo! Ikiwa Mungu ni ngao yetu, kwa nini tunateseka? (Hebu tuliangalie jambo hilo katika sehemu inayofuata.)

 

    1. Nani anayejaribu kujua kama imani yetu ni halisi? (Soma Ayubu 1:1 na Ayubu 1:8-11. Katika kisa cha Ayubu tunaona ni Shetani ndiye anayetujaribu, sio Mungu.)

 

      1. Ayubu anaelezeaje vifungu tulivyovisoma kuhusu utii na mateso? (Ayubu alitii na alibarikiwa sana. Hata hivyo, Shetani aliingilia kati kujaribu kuonesha kuwa imani ya Ayubu haikuwa halisi.)

 

    1. Kwa nini Shetani aruhusiwe kuingilia mibaraka yetu? (Soma 1 Petro 2:21. Wanadamu walichagua kuruhusu dhambi iingie katika dunia yetu. Yesu alipata mateso na kufa – kwa ajili yetu – ili kuikomesha dhambi. Hatuna msingi wa kulalamika tunaposhiriki sehemu ndogo ya mateso ya Yesu – mateso ambayo yangekuwa ya kutisha endapo Yesu asingeingilia kati ili kutuokoa. Kwa kuongezea, kama tu wakweli, mateso yetu mengi yanatokana na kutomtii Mungu “kikamilifu,”)

 

  1. Utii Kamili

 

    1. Soma 1 Petro 3:9. Kwa nini tuliitwa ili tuwe watifu? (“Ili tuweze kurithi baraka.”)

 

    1. Soma 1 Petro 3:10-12. Unalinganishaje vifungu hivi na vifungu tulivyovisoma kwenye kitabu cha Kumbukumbu la Torati 28? (Vinaonekana kushabihiana na Kumbukumbu la Torati 28.)

 

 

    1. Soma 1 Petro 3:13-14. Petro anasema kuwa kanuni ya jumla ji ipi? (Kwa ujumla haudhuriwi kwa kutenda jambo lililo sahihi. Lakini, hata kama unadhuriwa (kama ilivyokuwa kwa Ayubu), Mungu atakubariki kwa mateso yako yasiyostahili wala yasiyo ya haki.)

 

      1. Matokeo ya kuielewa na kuiamini kanuni hii ni yapi? (Kutokuwa na woga. Tunaweza kuwa na amani maishani.)

 

    1. Soma 1 Petro 2:9 na 1 Petro 2:15. Tuna sababu gani nyingine za kumheshimu Mungu? (Tunampa utukufu. Maisha yetu ya utii ni sifa kwa Mungu. Maisha yetu yatakinzana na “vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu.”)

 

    1. Soma 1 Petro 3:8-9. Tunawezaje kujijaribu kama tunaishi maisha ya utii? (Tunaishi kwa maelewano mazuri na Wakristo wenzetu. Maisha yetu yanaakisi upole (utu wema), upendo, huruma na unyenyekevu. Hatulipi ubaya kwa ubaya (uovu kwa uovu) au tusi kwa tusi.)

 

  1. Mbingu

 

    1. Soma 1 Petro 1:3-4. Yesu, katika neema yake kuu, ametupatia nini? (Uzao mpya katika “tumaini lenye uzima” na “urithi usioharibika, usio na uchafu au kunyauka.”)

 

      1. Tafakari jambo hili kidogo. Unaweza kuwa na kitu gani hapa kisichoweza kuharibika, kuchafuka au kunyauka? (Nilikuwa ninalifikiria jambo hili mapema juma hili. Jambo la kudumu ni kuwa na shule na kuyapa majengo jina lako. Kitu gani kinaweza kuyachafua majengo hayo? Jengo linaweza kuangamizwa kwa maafa (baa) ya asili. Shule inaweza kumwomba mtu fulani kuikarabati, na kuiita shule jina jipya kwa kuipa jina la mtu aliyelipia gharama za ukarabati. Panaweza kuwepo na madai ya wanafunzi kwamba jina lako liondolewe kwa sababu hawakubaliani na baadhi ya vipengele vya maisha yako.)

 

    1. Soma 2 Petro 3:10-13. Nini kitatokea mbinguni? (“Nyumbani!” Yatakuwa makao yako mapya. Dunia ya kale imeangamizwa. Mibaraka ya mali iliyoahidiwa katika Kumbukumbu la Torati 28 inateketea motoni na kupotelea kwenye moshi.)

 

      1. Soma Luka 12:32-34 na Mathayo 6:19-2 Hii inapendekeza mkakati gani wa kuhamisha mali uliyonayo sasa hivi? Unawezaje kuhakikisha kwamba haitaangamizwa?

 

  1. Nchi (Dunia)

 

    1. Soma 1 Petro 2:13-14. Wajibu wetu kwa serikali ni upi?

 

    1. Soma 1 Petro 2:15-16. Je, huu ndio upungufu kwenye maelekezo ya kutii mamlaka? (Petro anaonekana kuchukulia (sina uhakika kwa nini kutokana na mazingira na matukio ya maisha yake) kwamba serikali itatuambia kutenda yaliyo mema. Inaonekana hatimaye Petro anatuelekeza kuyatii mapenzi ya Mungu, ambayo ni kwamba tunapaswa kutenda mema.)

 

    1. Soma 1 Petro 2:17. Je, kifungu hiki kinafafanua wajibu wetu kwa mfalme na kwa Mungu? (Wakati “tunamheshimu” mfalme, “tunamcha” Mungu. Wajibu wetu mkuu ni kwa Mungu.)

 

 

    1. Soma 1 Petro 5:1-2. Hapa tunajadili mamlaka gani? (Mamlaka ya kanisa. Mamlaka ya kikanisa badala ya mamlaka ya nchi.)

 

    1. Soma 1 Petro 5:3. Mamlaka ya kanisa yanalinganishwaje na mamlaka ya nchi? (Wazee, mamlaka ya kanisa, wanapaswa “kutumikia” na “sio kuwa mabwana wakubwa” kwa washiriki wa kanisa.)

 

    1. Soma Matendo 15:12-13. Muktadha wa hivi vifungu ni upi? (Kanisa la awali lilikuwa na mabishano juu ya endapo waumini wapya wa mataifa wanapaswa kutahiriwa.)

 

      1. Kama ulikuwa unafuatilia alichokiandika Petro, unaweza kuchukua maamuzi gani? (Unaweza kudhani kwamba kwa kuwa viongozi hawakupaswa kuwa “mabwana wakubwa” kwa watu wengine, kila mtu anatakiwa kuchukua maamuzi yake katika jambo linalohusika.)

 

    1. Soma Matendo 15:19-20. Bado Yakobo anaongea hapa. Je, Yakobo ameenenda ki “bwana mkubwa” kwa kanisa la awali? Je, anafanya zaidi ya kutumikia? (Mfano huu unatusaidia kuelewa anachokisema Petro. Petro anatuambia kuwa viongozi wa kanisa hawapaswi kuenenda kama wafalme. Kwa upande mwingine, mfano wa Yakobo na kanisa la awali unaonesha kwamba viongozi wa kanisa wanaweza (na wanapaswa) kufanya maamuzi juu ya mabishano ya mafundisho ya kidini.)

 

      1. Kumbuka kwamba linapokuja suala la wafalme, Wakristo wanawajibika kumtii Mungu na kutenda kilicho sahihi. Je, ukweli huu pia unapaswa kutumika kwa viongozi wa kanisa? Vipi ikiwa unadhani kuwa viongozi wa dini hawayafuati mapenzi ya Mungu, na hawatendi kilicho sahihi? Lini uliona ubishani wa kiteolojia ambapo watu kutoka kila upande hawakudhani kuwa walikuwa wanajenga hoja upande wa Mungu. Kila mjadala wa mafundisho ya dini utakuwa na madai ya mamlaka ya Mungu katika pande zote mbili.)

 

        1. Unadhani kundi lililokuwa linashadadia tohara katika kanisa la awali lilikuwa linadhani kuwa linamfuata Mungu?

 

        1. Una maoni gani: je, hii inamaanisha kuwa hatupaswi kuwa na mtazamo wa pekee wa “kumfuata Mungu na kutenda kilicho sahihi” katika maamuzi ya viongozi wa kanisa?

 

    1. Hebu turejee nyuma kwenye maamuzi ya Yakobo. Soma Matendo 15:6. (Ni nani aliye sehemu ya kundi lenye kutoa maamuzi? (Hii inaonekana kuzungumzia mambo mengi zaidi ya Yakobo pekee.)

 

    1. Soma Matendo 15:7-9. Hoja ya Petro ni ipi? (Anasema Roho Mtakatifu anabariki kazi ya Mataifa wasiotahiriwa.)

 

    1. Soma Matendo 15:12. Hoja ya Paulo na Barnaba ni ipi? (Kwa mara nyingine, wanazungumzia uwezo wa Roho Mtakatifu.)

 

    1. Sasa, ngoja niulize tena endapo panapaswa kuwepo kwa jambo lisilo la kawaida la “kumfuata Mungu na kutenda kilicho sahihi” katika maamuzi ya viongozi wa kanisa? (Ikiwa Roho Mtakatifu ameonesha kwa dhahiri kinachotakiwa kutendeka tunapaswa kufuata maelekezo yake. Viongozi wa kanisa, ambao wanatakiwa kutumikia, wanapaswa kufuata maelekezo ya Roho Mtakatifu.)

 

    1. Rafiki, Petro anataka uishi maisha yanayokupa baraka na kumpa Mungu utukufu. Anataka kuyarefusha maisha yako katika umilele wa kuwa na Mungu. Je, utamkaribisha Roho Mtakatifu akuongoze uyaishi maisha ya namna hiyo?

 

Juma lijalo: Tutaanza mfululizo mpya unaoitwa “Injili Katika Wagalatia.”